Thursday, January 16, 2014

...MWIZI...

10th January, 2014, Ijumaa

“Mwizii, mwiziiii, mama mwiziiiii, kaniibiia mwiziiiiiiii….nisaidieniii kaniiibia, mwiziiiiiiiiiiiiiiiiiiii” Niliisikia sauti ya kike ikiita kwa nguvu. Haikuwa ikitokea mbali na nilipo. Nikageuka kuona huyu mwizi yuko wapi nami nione kama nitaweza kumsaidia mrembo huyu.

Niliona vijana kadhaa pembeni yangu wakiokota mawe. Ghafla, nilihisi kitu kizito kikinipiga maeneo ya kichwani….

26th October, 2012, Ijumaa

Ngo ngo ngo…Mlango wa ofisini uligongwa.

Mimi: “Karibu”

(huku akifungua mlango) “Asante” iliitikia sauti nyororo, nyepesi, laini ambayo kwa zile flash-seconds chache kabla sura haijajitokeza, kichwani kwangu nilikuwa tayari nimeshatengeneza sura na umbo la mhusika hata bila ya kumuona.

Aliingia binti mmoja mweupe, mrefu wa wastani. Alivalia blauzi nyeupe ambayo ukiikazia macho utaona vyema muundo wa tochi mbili zilizosimama vyema kifuani pake zikiwa zimeshikiliwa na bra ya buluu mpauko ambayo ilivaliwa zaidi kama urembo kuliko kutimiza kazi yake. Chini alivaa sketi nyeusi ndefu iliyoshuka vyema na mwili wake mwembamba lakini uliojengeka sehemu stahiki hadi kuja kuungana na kiuno chembamba kilichoonekana dhahiri kutokana na kuchomekewa kwa ile blauzi.

“Habari ya saa hizi kaka”

“Nzuri, karibu, karibu ukae” (huku nikimuonesha kiti cha pembeni na kumkaribisha)

Kwa kweli hapa nilikumbuka mafundisho yote ya huduma kwa mteja na nilijitahidi kuweka na madoido mengine kuhakikisha kuwa mteja wangu huyu anaridhishwa na huduma yangu hadi atakapoondoka ofisini pale. Kabla sijaanza kumuuliza shida yake alianza kuongea.

“Naitwa Asha Daudi, natokea  Kikulacho Company. Tunatangaza bidhaa zetu za king’amuzi hiki cha Kikulacho (huku akitoa makaratasi na kunikabidhi). Ni king’amuzi kizuri, and we offer competitive prices. Ukikubali kununua na kujiunga nasi basi utafungiwa king’amuzi chako bure na kupewa huduma ya matengenezo kwa miezi mingine mitatu kama kutatokea tatizo lolote.” Nilivutiwa na jinsi mrembo huyu alivyokuwa akiongea.

“Asante sana dada, tena ni kama bahati maana siku za hivi karibuni nilikuwa nachagua kipi king’amuzi bora kwa nyumba yangu.” Nilijitahidi kutupia macho kwenye karatasi alizonipatia Asha. Akili yangu ya kibazazi ilikuwa ishawaza pengine. 

“Ooh naona hapa premium ndo mnaonesha na channel za michezo eeh.” Niliuliza vimaswali vya hapa na pale ambavyo ilimbidi asimame na kuja kunielekeza kwa ukaribu zaidi. Ni hatua zisizozidi sita kutoka kiti alichokuwa amekalia kuja nilipo lakini alizitembea kama vile yupo kwenye mashindano ya ulimbwende. Alikuja na kuinama mbele yangu huku akiacha sehemu ya kifua ikiwa wazi na kunifanya hata nisimuelewe alichokuwa akikisema. 

“…ndo hivyo iko, wewe ulikuwa unafikiria kipi hasa?” Ndicho nilichobahatisha kumsikia.

Ilibidi nijibaraguze na kazi hivyo nikamuomba aniachie karatasi zile nifanye maamuzi baadaye kwani nina kazi ‘pressing and urgent, running towards its deadline’ nilitakiwa kuifanya kwa ajili ya ‘final presentation’ kwa ‘board of trustees’ hivyo nisingeweza kutafakari na kufikia uamuzi kwa wakati ule.   Alinishukuru na kuaga kuondoka.

“Errr…samahani!” (Nilimwita kabla ya kufungua mlango)

“Bila samahani kaka” (aliitika kwa tabasamu la mbali lililonifanya nipaliwe kwa kumeza fundo kubwa la mate ya tamaa)

“Niandikie namba yako hapa kwenye karatasi yako basi tutaongea baadaye nikipata nafasi ya kuangalia hizi karatasi in case nitakuwa na swali” (nilijibaraguza na maelezo)

Alirudi na kuniandikia namba zake kisha akaniaga na kuondoka huku nyuma akiniachia simanzi la moyo na akili ilianza kutafakari ni mbinu gani nitatumia kumpata binti huyu, Asha!

Haikuchukua siku nyingi kwani Jumapili tu nilimpigia simu Asha na kupiga naye stori mbili tatu. Nilimjulisha kuwa ningependa kufahamu jinsi ya kulipa na vitu kama hivyo na aliniahidi kuwa angepita tena ofisini siku inayofuata kunipa malekezo zaidi.

Haikuwa hadi Jumatano ambapo Asha alikuja nami nikamuomba kwa kuwa sikuwa na kazi nyingi basi twende tukapate chakula cha mchana pamoja. Kwa shingo upande alikubali kwani alisisitiza kuwa anatakiwa kwenda ofisini kurudisha majibu ya kazi za siku hiyo. Ushawishi wangu pia haukuwa haba hivyo alikubali. Tuliongea mengi yasiyohusu kazi na ndipo nilipofahamu kuwa alikuwa amemaliza shahada yake ya kwanza ya masomo ya utawala wa rasilimali watu. Tatizo kubwa lilikuwa kupata ajira kwa fani aliyosomea hivyo wakati akisubiria kuitwa kwenye usaili wa kazi alizo-apply hakuwa na budi kujishikiza hapo kwenye kampuni ya ving’amuzi ya ‘Kikulacho.’

Kwa kifupi alitangaza dhiki. Ndipo ubazazi wangu ukajua njia ya kupitia kutimiza adhma yangu kwa Asha. Tulimaliza kula na kabla ya kuagana nilimpatia elfu hamsini na kumsisitizia kuwa itamsaidia kusogeza siku kwani nafahamu kuwa commission anayolipwa haitoshelezi mahitaji yake. Alinishukuru sana. Tukaagana na kuendelea na shughuli zetu kila mmoja.

Tuliendelea kuwasiliana sana kwa simu huku akiulizia lini nakuja kulipa king’amuzi. Hakujua kuwa hata mpango wa kulipia king’amuzi sikuwa nao. Tulizoeana mpaka kufika wakati alikuwa akija ofisini jioni baada ya muda wa kazi tunaenda Mary’s, au breakpoint tunapata mbili tatu huku tukipiga stori za hapa na pale tukingojea foleni zipungue. Alikuwa tayari amenichukulia kama rafiki yake na akilini mwangu nilishaamua kuwa ni muda wa mashambulizi.

Nilimchombeza kuwa Ijumaa moja twende zetu Kigamboni (kipindi hiki nilikuwa bado nikiishi Gongo la Mboto, Kitunda). Mwanzoni alitaka kusita lakini baada ya ushawishi mwingi na ahadi za uongo za ‘sitofanya lolote usilopenda nifanye’, alikubali.

Baada ya wikiendi ile, Asha alifanya kosa kubwa…alijihalalishia uchumba! Alikuwa akiwafahamu baadhi ya rafiki zangu ambao mara nyingi tulikuwa tukikutana jioni nikiwa naye. Na kama kawaida yetu kila utakayekuja naye wao wanamuita, ‘shem!’ Asha hakulifahamu hilo, alidhani alikuwa ‘shem’ peke yake. Niliendelea kujilia vyangu kiulaini kwani sasa ameshakuwa shem wao. 

Tatizo lilianza kuja nilipotaka uhuru wa kufanya ‘yangu’. Asha alishakolea kwangu kiasi kwamba akataka kuninyima uhuru. Ulikuwa ni wakati wa kukata kamba. Kwa mantiki hyo kulikuwa na haja ya kusitisha mkataba haraka iwezekanavyo kwani kulikuwa na wateja wengine in-line wakingojea kuhudumiwa nami. Kwa uzoefu wangu nilijua mbinu pekee ya kumuacha Asha ilikuwa kukatisha mawasiliano haraka iwezekanavyo.

Kwanza nilijipa safari ambapo huko ‘safarini’ hakukuwa na mtandao ila sasa hizo baby na honey kwa kweli zilinikera. Alikuwa akiota ndoto za mbali sana. Nilirudi ‘safari’ ila niliendelea kukaa kimya hadi alipoona mwenyewe hapa niliuziwa cover la ‘Olympus has Fallen’ ilhali ndani kuna CD ya King Mzee Majuto.

Baada ya ukimya usio na maelezo na meseji zisizojibiwa, alijikatia tamaa. Kama kawaida alinitumia ujumbe mfupi wa vitisho kuwa lazima atalipiza kisasi siku moja kwa niliyomfanya. 

“Ha ha ha” nilijichekea moyoni kwani kama ni visasi basi hakika ningekuwa na kijiji cha watu wenye kutaka kulipa kisasi kwa orodha ya niliowapitia na kuwaacha kwenye mataa. Nilifarijika zaidi nilipopata habari kuwa Asha amepata kazi mkoani Dodoma na hivyo hatutakutana tena jijini hapa hata kwa bahati mbaya.

Maisha yalisonga mbele…

10th January 2014, Ijumaa 1550hrs

Nilifunga ofisi mapema kwa matarajio ya kuwahi nyumbani kujiandaa na safari ya Morogoro kesho yake. Ilikuwa safari ya kikazi lakini pia nilikuwa na miadi na Clara, mwanafunzi wa Mzumbe ambaye tulikutana juzi juzi Dar walipokuwa likizo za Christmas na mwaka mpya. Niliipania sana safari hii.

Ni kwa sababu hiyo niliamua kuacha gari ofisini ili kesho yake nisipange foleni ya kungojea pantoni niwahi tu safarini. Hivyo nilijikuta nikitembea kuelekea ferry. Kutokana na matengenezo yanayoendelea ya barabara za mabasi ya BRT eneo hilo kuna vumbi sana hivyo inakubidi kutembea ukiwa umefungua macho kwa mbali.

Nikikaribia kabisa pale ambapo pikipiki na bajaji nyingi hupaki niliiona sura ambayo ilinivutia macho. Binti mmoja mrefu wa wastani, mweupe, amevalia sleeveless top ya pink na suruali ya buluu. Nilijikuta nikibadili uelekeo ili walau nimfikie binti yule. Alikuwa katika msongamano wa watu waliokuwa wametoka kwenye pantoni wakielekea mjini. Akili yangu iliwaza jambo moja tu, ‘nikifanikiwa kumsalimia tu…’

Kwa bahati macho yetu yaligongana, na ni kama alikuwa amesoma mawazo yangu kwani naye alijitahidi kupenya kwenye msongamano ule kunielekea mimi. Nilitabasamu moyoni. Tulielekeana huku nikimkazia macho yenye tabasamu la mbali. Alikuwa ameyakaza macho yake kwangu kwa jinsi ambayo kwa wakati ule sikuwa nimeelewa sababu. 

Ha! Haikuwa sura ngeni! Oh maama…alikuwa Asha Daudi!!!! Katika hali ile ya mshituko sikujua hasa lengo langu lilikuwa kumpa mkono au kumkumbatia, ila na yeye alikuja hadi kunigonga kabisa. Ndipo ghafla nikazisikia zile kelele…

“Mwizii, mwiziiii, mama mwiziiiii, kaniibiia mwiziiiiiiii….nisaidieniii kaniiibia, mwiziiiiiiiiiiiiiiiiiiii” Niliisikia sauti ya kike ikiita kwa nguvu. Haikuwa ikitokea mbali. Nikageuka kuona huyu mwizi yuko wapi nami nione kama nitaweza kumsaidia mrembo huyu. Alikuwa ni Asha anapiga kelele za kuibiwa. Sikuelewa ameibiwaje na mimi nilikuwa karibu naye kabisa na nisimuone mwizi yule. 

Ni hadi aliponyoosha mkono kunielekea ndipo nilipoelewa…alikuwa amedhamiria, alipanga!

17th January, 2014

Ni leo nimeruhusiwa kutoka hospitali kwa kipigo cha mbwa mwizi nilichokipokea siku ile. Kama sio askari waliokuwepo karibu na mahali pale, basi leo ningekuwa na jina lingine. Nimeambiwa natakiwa kwenda kujibu kesi mahakamani. Nashindwa kuelewa kama hakimu ataniamini nitakapomueleza hadithi hii.

Wasalaam wapendwa,
Mentor.

No comments:

Post a Comment