Vita Dhidi ya Rushwa ya Ngono Mashuleni
Siku za nyuma, mwaka 2024, kulizuka mjadala mkubwa sana kwenye mitandao ya
jamii hasa twitter. Mjadala huu ulihusu rushwa ya ngono vyuoni baada ya Mhadhiri
wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kukutwa na mwanafunzi hotelini. Sikubahatika
kuiona hiyo video mpaka sasa lakini tukio hilo limeniwazisha na kuninyima amani
kwa muda mrefu.
Wengi walitoa maoni yao kwenye mitandao hiyo na mimi nilijaribu kutoa ya
kwangu hadi kufikia kutukanwa. Nilishtushwa na kusikitishwa kwa mambo mawili;
kwanza, aliyenitukana ni mtu niliyekuwa nikimheshimu kitaaluma kama Mwanasheria
na wakili msomi na niliheshimu maandishi yake, walau mtandaoni, maana
kiuhalisia hatufahamiani. Lakini pili, ni kwa jinsi ambavyo hakutaka mjadala wa
kistaarabu na kuishia kunitukana.
Hata hivyo, wahenga wanasema, ‘kuvunjika kwa koleo si mwisho wa uhunzi’.
Mjadala huu bado umeendelea kuniwazisha.
Wapo waliosema kuwa lawama wapewe wahadhiri 100%, wapo waliosema lawama
wapewe wanafunzi 100%, wapo waliokuwa na mtazamo wa 80/20% kila upande, na wapo
waliosema ni 50/50%. Na kila kundi lilikuwa na sababu zake.
Ningependa kuanza na mfano aliotoa mmoja wa wachangiaji huko twitter,
alisema, “Hawa wahadhiri wa kiume mnaowaona na kuwasema humu mitandaoni
wanaonekana kama maharamia, wanapitia mambo magumu sana kwenye hii kazi ya
kitaaluma hususani linapokuja suala la mwanafunzi wa kike, yasikieni tu. These
girls of nowadays wana technicalities nyingi mno kwenye haya mambo.”
Mwingine akaandika, “’Hawa
mabinti usiwaone hivi aisee, kuna siku niliwahi letewa ofisini kwangu mashati
mawili, saa, soksi, na suruali za kadeti za bei mbaya tu, halafu akaachiwa
secretary wangu na maelezo kuwa akija Sir mpatie mzigo wangu’ jamaa yangu mmoja
mhadhiri aliwahi nisimulia hii issue”
Rushwa ya ngono mashuleni inalelewa na kukuzwa na wahadhiri wenyewe na si
wanafunzi. Na hapa naomba niweke kumbukumbu sahihi kuwa rushwa ya ngono
inafanywa na wahadhiri wa jinsi zote mbili, wa kiume na kike.
Voltaire, mwanafilosofia, aliwahi
kusema, “With great power comes great responsibility.” Winston Churchill
alirejea msemo huo pia akisema, “The price of greatness is responsibility.”
Tafsiri sisisi inaweza kuwa, “Kwa
kila mamlaka/ukubwa kuna wajibu wake.”
Kwa kusimamia maneno haya, ni dhahiri kuwa hakuna sababu inayomfanya au
kumruhusu mhadhiri kuwa mwathirika (victim) wa rushwa ya ngono. Rushwa yoyote
inatokana na mojawapo ya sababu zifuatazo;
-
Mtoaji
wa rushwa kuwa na hitaji la kupewa kipaumbele dhidi ya wengine wenye sifa sawa
au zaidi yake,
-
Mtoaji
wa rushwa kutaka kuharakishiwa jambo,
-
Mtoaji wa rushwa kutaka upendeleo asioustahili,
au
-
Mtoaji wa rushwa kutishiwa kunyimwa haki/stahiki
yake asipotoa rushwa.
Kwa upande wa mpokeaji,
atapokea tu endapo anachopewa kina manufaa kwake kwa wakati huo lakini hakimpi
haki au faida yoyote ya moja kwa moja na kazi yake.
Kwa misingi hii, rushwa ya ngono mashuleni
hutokea kwa; Mwalimu kumtaka mwanafunzi kimapenzi bila ridhaa ya mwanafunzi na
hivyo mwanafunzi kushawishika kukubali kwa aidha kuchoka usumbufu, kutishiwa
aidha kufeli au kupunguziwa alama za mitihani, AU mwanafunzi kumshawishi
mhadhiri kuwa akimsaidia jambo lake lihusulo masomo yake, basi atamzawadia
mwili wake kama shukrani.
Hivyo basi, tukitaka kutokomeza
rushwa ya ngono vyuoni ni lazima tuwatake walio na mamlaka kuwajibika zaidi ya
wanavyowajibika sasa. Tusimbebeshe lawama mwanafunzi kwa kuwa tu, alimpelekea
mhadhiri zawadi. Kwa mamlaka aliyonayo alipaswa kukataa zawadi zile kwani alijua
zina lengo gani. Tusimbebeshe lawama mwanafunzi eti kwa kuwa ‘inajulikana
mwanafunzi mwenyewe ni malaya’. Kwani malaya akibakwa inaondoa kosa la jinai la kubaka kisa tu ni malaya? Tusipeleke
lawama kwa mwanafunzi kuwa angekataa kwani angebakwa? Mimi ninajua mabinti
waliopunguziwa alama kwenye mithani yao kwa kuwa tu walikataa kulala na
Mwalimu. Tusimbebeshe mwanafunzi lawama eti kwakuwa ana zaidi ya miaka 18 hivyo
ni makubaliano ya watu wazima.
Ni ukweli kuwa mtoaji na mpokeaji wa rushwa wote wana makosa. Lakini tukianza kuwatengenezea visingizio
wahadhiri hawa, tutakuwa tunadhoofisha vita hii. Tutakuwa tunataka kuhoji na
kumfanya mwanafunzi kuwa mkosaji. Tuchukue kipimo cha Mwalimu Nyerere kuwa Mtumishi
wa Umma hutakiwi hata kushukiwa kujihusisha na vitendo viovu kwenye jamii.
Tutengeneze njia nzuri na salama za wanafunzi wanaoombwa rushwa za ngono na
walimu kuweza kutoa taarifa na taarifa hizo kufanyiwa uchunguzi usio na uonevu
wala upendeleo dhidi ya malalamiko yao na itakapobainika kuwa ni kweli basi
tuwe na sheria madhubuti kuhakikisha mhusika anaadhibiwa vikali ili iwe funzo
kwake na wengine wenye tabia kama zake. Hii itaondoa hofu ya mhadhiri kuhisi
atasingiziwa lakini pia itaondoa hofu ya mwanafunzi kuona kama atachukuliwa
kama mkosaji akitoa taarifa (victimized). Zaidi sana italinda utu wa wote
wawili tofauti na kinachoendelea sasa hivi cha kufumaniana kwenye vyumba vya
hoteli.
Kwa namna yoyote, siondoi umuhimu wa elimu kwa vijana wetu wa vyuoni
kuelimishwa juu ya kujikinga na vishawishi hivi kwa kufanya nafasi yao kwenye
masomo yao, kuweza kusema hapana inayomaanisha hapana, na kujua njia sahihi za
kutoa taarifa endapo itahitajika. Na elimu hii pia ianzie chini; kuwafunza
watoto wetu kuwa waaminifu, kuwafundisha watoto wetu kukataa rushwa,
kuwafundisha watoto wetu kujithamini, kujiheshimu, na kuwa na maadili
yawapasayo kuyaishi endapo watakuwa wanafunzi au Wahadhiri au Watumishi mahali
popote na kukumbwa na vishawishi kama hivi.
Mjadala huu uliibua maoni ya watu wengi kwenye sekta nyingine za kazi hasa
sekta ya afya jambo ambalo hata mimi sikuwa nikilifahamu. Lakini bado mtazamo wangu ni ule ule;
tutengeneze njia salama ya kutoa taarifa na kuzichunguza kisha tuwe na sheria
madhubuti zenye kutoa adhabu kali kwa wahusika wa rushwa hizi za ngono.
Hakuna, na narudia, hakuna kisingizio cha Mhadhiri, Mwalimu, Askari,
Daktari, Mtumishi wa Umma kusema alishawishiwa kupewa rushwa ya ngono (na
rushwa nyingine) na kwamba agawane lawama na mtoaji. Kwa kukubali nafasi na
mamlaka uliyonayo, unao wajibu mkubwa zaidi kuitetea nafasi hiyo na kuitumikia
kwa heshima na nidhamu kubwa.
Tukikubali kumtengenezea visingizio mhadhiri, basi tusimseme mtumishi
mwingine yeyote anayeshawishika kupokea rushwa - ya aina yoyote ile - kwani nao
kama walivyo wahadhiri, ni binadamu wenye tamaa za mwili na wanaweza kushawishika
kwa fedha au kingono.
Wasalaam wapendwa,
Mentor.
No comments:
Post a Comment