Saturday, June 25, 2016

SITAKI DAWA



SITAKI DAWA
Jumamosi, 25/06/2016
Nawaza nianzie wapi kuelezea kilichonikuta nashindwa, lakini hasa ni kukosa maneno ya kukielezea. Nimetamani nikae kimya, nisiseme, maana ninafahamika na wengi na itaniharibia picha yangu kwenye jamii. Nimetafakari sana kuchukua maamuzi magumu lakini nfasi yangu haikuumbwa hivo, nimeshindwa. Labda ningezaliwa Mhehe, lakini Mchagga mimi hata vidonge vya 'piriton' vilikuwa shida kumeza.

Lakini nimeamua nitasema. Sijui baada ya kusema nini kitatokea, sijui jamii itanichukuliaje, ndugu jamaa na marafiki watasemaje au labda watanitenga…lakini nitasema.

Wazazi wangu – MNISAMEHE! Zaidi ya yeyote yule, nimewaangusha. Mlikuwa na mategemeo makubwa juu yangu. Mmenisomesha kwa gharama kubwa na mlikuwa na matumaini ya mimi kufika mbali. 

Mlioniita Mentor – MNISAMEHE! Najua ni wengi walioniona kama kijana wa mfano, kaka na ndugu…mnisamehe kwa kuwaangusha. Sitamsingizia shetani wala mtu mwingine yeyote kwa kosa langu.

NIMEATHIRIKA! Na sijivunii…

July, 2015

Naamini ni wakati huu. Kulitangazwa nafasi za masomo nchini Uingereza chini ya ufadhili wa Commonwealth (Commonwealth Scholarships 2015). Nami nilikuwa nimejiwekea malengo kuwa hadi mwaka 2016 ni lazima nikasome masomo yangu ya Uzamili (Masters Degree) hata ikibidi kwa kujilipia. Nilitembelea tovuti tofauti tofauti nikitafuta ufadhili kwa ajili ya masomo yangu. Hakuna tangazo lililotolewa ambalo sikuliomba. Fulbright, Mwalimu Nyerere, DAAD, World Bank, IMF, n.k n.k niliomba zote. Nilikuwa na malengo ya kwenda kusoma masomo ya Usimamizi wa Miradi au Sera za Umma na Utawala. Ndoto yangu ilikuwa moja tu: SIKU MOJA NIWE KATI YA WAFANYA MAAMUZI KATIKA NCHI HII

Nilichoka kuwa mtu wa kutengeneza mifumo ya TEHAMA (programmer) kila siku halafu aidha fedha zinaliwa au mifumo inawekwa kwenye makabati. Nilichoka kuhusishwa kwenye miradi isiyo na kichwa na miguu, miradi isiyoangalia vipaumbele vya Taasisi au Nchi. Nilichoka! Nikasema nitaachana na masomo yangu ya Sayansi ya Kompyuta nikasome masomo yatakayonifanya niwe mtunga sera na mtoa maamuzi. FUCK ME!!!! (mnisamehe am so mad at me)

Wakati huu ndipo kulipotangazwa nafasi hii ya Commonwealth. Nakumbuka nililiona tangazo kupitia tovuti ya TCU na ilikuwa imebaki wiki moja au mbili hivi kabla ya tarehe ya mwisho kwa hapa kwetu. Nilijipinda ofisini kuandika insha kama tatu kuelezea kwa nini mimi niipate nafasi hii na si mwingine. Niliandika kutoka moyoni. Nilifanikiwa kumaliza mapema nikatoa nakala kama walivyoelekeza; za kupeleka Wizara ya Elimu na za kutuma kwa barua pepe.

Siku, wiki na miezi vilipita nami nikaitwa kwenye usaili, nikaenda kufanya mitihani ya Kiingereza ya IELTS pale ubalozi wa Uingereza, nikafaulu vizuri.

Alhamisi, 23 Juni 2016 - Juzi

Nilipewa majibu kuwa nimechaguliwa pamoja na wenzangu wawili kwenda Uingereza (Chuo sitokitaja) kwa ajili ya masomo ya Uzamili katika Usimamizi wa Miradi kuanzia mwezi wa tisa. Nilifurahi sana, nikapiga magoti ofisini nikamshukuru Mungu kuwa mwaminifu kwangu. Nilimuomba mwaka huu niende shule na amenijibu. Tena kaniongezea baraka kwa kuwa ninapewa ufadhili wa asilimia mia (100%). Hakuna hata senti yangu nitakayotumia katika maosomo yangu hayo.

Jana asubuhi nilitumiwa mkataba wangu pamoja na fomu za afya ambazo nilitakiwa kuzijaza na kuzirudisha ubalozi wao Jumatatu kwa ajili ya mipango mingine; visa na kuomba ruhusa kwa Katibu Mkuu Kiongozi (serikali ya awamu ya tano hii!) 

Kwa ile hamu niliyokuwa nayo wala sikuweza kubaki tena ofisini nikajiondoa kuelekea Mnazi Mmoja maana nilijua hilo sio suala gumu. Nilishazoea kibongobongo hakuna kufanya vipimo na kwa kuwa nilishaulizia kuhusu visa za Uingerea nilifahamu huwa hawafanyi vipimo vya afya vingine zaidi ya kile kilichoandikwa kwenye ile fomu. Hivyo niliamini wala lile zoezi lisingechukua zaidi ya nusu saa. Niliingia kwenye ATM ya bwana Kimei pale Posta nikachukua fedha ya kutosha kwa ajili ya kumshukuru daktari atakayenisainia fomu zangu.

Nilimkuta mmama mmoja!dah nikamsalimia na kumueleza kilichonipeleka pale. Nilishangaa alipochukua kikaratasi chake na kuanza kujaza vipimo ambavyo nilitakiwa kwenda maabara kupima kabla hajanijazia fomu yangu. Nilitamani kuondoka lakini nikakumbuka ameshaichukua fomu yangu na alijua ninataka kuondoka akaiweka kwenye droo na kunikabidhi kile kikaratasi nielekee maabara. Nilijaribu kumuomba kwamba nimetoroka kazini anisainie tu na kupiga muhuri nami ningemshukuru vizuri tu. Alikataa na kunitaka niende kupima.

Niliondoka huku nikisoma kile kikaratasi ila nilipofika kwenye hili neno PITC nikashtuka kidogo. Ufadhili (scholarship) nautaka na vipimo sivitaki nifanyeje sasa, ikanibidi nielekee maabara. Nikaelekezwa kwenye dirisha la kulipia nikalipa (nilisahau kabisa kwamba nina bima ya afya hiyo jana). Nikarudi kwenye kiti changu kusubiri wakati wangu wa kuitwa.

Palikuwa na makelele na kulikuwa na nesi mmoja anaita watu majina. Namkumbuka kwa kuwa alikuwa na sauti kubwa kuliko mwili wake. 

MAGRETH! MAGRETH!” aliita kwa nguvu. –kimya

Akaendelea kuita jina lingine, “JACKLINE!” “JACKLINE!

Mh! Haya majina mawili kwa pamoja yakanikumbusha Changanyikeni.

Sikumbuki siku kamili!

Nilikuwa na rafiki yangu tuliyeshibana sana toka utotoni, Arnold. Huyu jamaa ndiye aliyenifundisha ule msemo wa KUPATA UKIMWI MPAKA UWE UMELOGWA. Nami niliuamini maana michezo niliyoicheza ujanani tena pekupeku sikuwa nimeathirika, kweli mpaka uathirike ni lazima ulogwe. 

Ndiyo, kuna nyakati nilijua sijaathirika kabisa kwa kuwa mara nyingi mabinti niliokuwa nao kwenye mahusiano walikuwa wakiniambia. Nakumbuka huyu mmoja ambaye alinifuma nikiwa choo cha klabu na mwanamke mwingine ambaye hata jina sikuwa nikimfahamu. Alinikuta nikifanya naye mapenzi pasi na kinga. Nilikuwa nimeshazoea. 

Huyu ndo alinifumbua macho siku moja miezi michache baada ya kuachana nami kuwa kitu cha kwanza alichoenda kufanya baada ya usiku ule ni kwenda kupima ambapo alipojikuta hakuathirika alishukuru sana. Ndipo nami nikagundua kumbe sikuathirika. Niliifanya kama mchezo kwamba kila binti niliyeachana naye; kumuacha au mara nyingi yeye kuniacha, baada ya miezi michache nitamuuliza kama amepima na mara nyingi huniambia wako poa. Nami hujua niko vizuri.

Ah! Jacky na Mage

Nakumbuka ilikuwa siku niliyotoka ubalozi wa Uingereza ambapo niliambiwa nimepita usaili na nijiandae tu kwa ajili ya mitihani ya Kiingereza. Baada ya kufanya utafiti mfupi niligundua mitihani ile si migumu na kwa watu wote tuliopita usaili mimi nisingeweza kukosa ufadhili ule kwa kamtihani kale karahisi ka kiingereza. 

Nilimpigia simu Arnold na kumuambia tukasherehekee. Tulienda Samaki Samaki ambapo tulikutana na Jacky na Mage, tulisoma nao O-Level huko Moshi. Tulipiga stori sana na kwa kuwa nilikuwa nasherehekea mimi ndo nilikuwa mnunuzi. Walikunywa vya kutosha kiasi kwamba wakati wa kuondoka wale mabinti hawakuweza kwenda peke yao. Ilikuwa kazi rahisi sana kuwashawishi twende kwangu Changanyikeni kwa kuwa pia ilikuwa ni siku ya Ijumaa. Tuliingia kwenye kausafiri changu hao mpaka Changanyikeni. 

Safari moja ikapelekea nyingine na yaliyotokea kule – sijivunii – na sitayaelezea na hatukuwa na kinga yoyote. Na wala siwezi kusingizia ulevi maana mimi huwa situmii kilevi chochote.

Mentor! Mentor!”

Sauti ya nesi yule ikiniita ilinishtua kutoka kwenye dimbwi la mawazo. Ulikuwa ni wakati wangu kwenda kwenye vipimo.

Nilinyanyuka na kuelekezwa kwenye chumba kingine ambapo nilipoingia sikukuta hata dalili za sindano. Kumbe ilikuwa kwa ajili ya vipimo vingine vilivyokuwa kwenye karatasi ile. Nilipima uzito, urefu, pressure, na mengine kama hayo kisha nesi akaniambia nirudi kukaa kwenye benchi.

Hapo akili yangu ikaniambia kuwa kinachofuata sasa ni Ukimwi. Nilikaa nikitafakari kama kweli ninaweza kuwa nimeathirika. Akili yangu ikakataa.

Usiku wa Mwaka mpya 2016

Najua wengi mnaonifahamu hamtaamini mkisoma hapa – MNISAMEHE! Wengi walinifahamu kama kijana Mkristo safi ninayeenda kanisani kila Jumapili. Hata kanisani kwangu ni mmoja wa viongozi wa vijana – nafasi ambayo niliitumia vibaya kuendeleza tabia yangu mbaya chini ya kapeti. 

Nilienda kwenye mkesha wa mwaka mpya. Tuliimba na kusherehekea sana na moyoni mwangu nilijiwekea malengo kuwa mwaka huu mpya nimtafute binti mmoja nitakayempenda na kutulia naye maana umri nao haunisubiri. 

Nilidhamiria kupunguza kwa kiasi kikubwa tabia zangu mbaya hasa ukizingatia mema mengi ambayo Mungu amekuwa akinifanyia bila kustahili kwangu. Ni katika kuwaza huku ndipo macho yangu yalipodondoka juu ya msharika mmoja. Hadi wakati tunatoka ibada usiku ule tulikuwa tumeshafahamiana vya kutosha. 

Itoshe kusema tu kuwa hatukufanikiwa kwenda kwenye ibada asubuhi ya tarehe 01/01/2016 kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wetu. Na hatukutumia kinga. Ni katika kuwaza huku ndipo nilipokumbuka kuwa juzi juzi tu alikuwa akiumwa na hakutaka kuniambia anaugua nini. “Atakuwa ameathirika?” nilijiuliza. Lakini nikajifariji kuwa KUPATA UKIMWI NI HADI ULOGWE. Ni nani wa kuniloga mimi Mentor, mtu wa watu, kwa kosa lipi nililomfanyia?

Jina langu liliitwa tena na kwenda kwa ajili ya vipimo vingine vilivyohusisha damu kuchukuliwa.

Nilitamani kuondoka pale kwani sikuwa nimeomba ruhusa ofisini lakini pia nilitakiwa kuondoka na fomu zile. Ilinibidi kusubiria.

Akili yangu ilikuwa ikisafiri mbali. Nilijiuliza maswali mengi kuhusu afya yangu ambayo sikuwa nimewahi kujiuliza kabla. Nilifanya mambo yangu mengi kwa siri kiasi kwamba ni vigumu mtu yeyote akihadithiwa haya kuyaamini. Lakini kwani UKIMWI unawapata waliofanya kwa wazi? Lakini hapana mimi siwezi kuwa nimeathirika. Kutoka kwa nani labda? 

Nikamkumbuka Amina, huyu alikuwa mdada wa usafi ofisini. Kama tabia yangu nimezoea kusalimia kila mtu na huyu dada tulikuwa tukikutana asubuhi wakati naingia ofisini hakukosa salamu yangu. 

Pamoja na tabia yangu ya kupenda kuwahi ofisini hakuna siku niliyowahi kwenda ofisini nisikute ameshafika. Tukazoeana sana. Nami kidogo kidogo nikaanza kumzoea na kumchokoza kwa vimaneno vya hapa na pale. 

Kuna zile siku unaamka mapema, unajisikia vizuri, unaoga unavaa unaingia kwenye gari unaondoka kwenda kazini mapema ukitegemea kutakuwa na foleni kubwa kumbe unapofika barabarani unatumia robo saa tu kufika ofisini. Hii siku ilikuwa hivyo. Na nilipofika saa kumi na mbili kasoro bado nilikuta Amina amekwishafika. Na kwa bahati zaidi alikuwa akifanya usafi ofisini kwangu. 

Sitaki kuelezea zaidi lakini itoshe kusema usafi uliishia palepale. Na hatukutumia kinga. Baadaye Amina alikuja kuzushiwa maneno kuwa anatembea na mabosi wangu wengine na eti ameathirika hivyo akafukuzwa na sikumuona tena. Sikuweza kumuuliza kama alipima au la! 

Lakini hapana, wakati ninakutana na Amina nilikuwa na rafiki wa kike, Hamida, na Hamida tulipoachana alienda kupima na hakukutwa na virusi. Nilitabasamu kugundua kuwa niko vizuri.

Lindi hili la mawazo lilikatishwa tena na nesi yule yule aliyeniita nyakati zilizopita. Niliiangalia saa yangu iliyonionesha kuwa ni saa mbili zimepita tangu nifike pale.

Niliingia kwenye chumba ambacho nilijua tu ni kwa ajili ya ushauri. Nilimwomba nesi aniandikie majibu yangu kwenye kile kikaratasi pamoja na yale majibu mengine niwahi kwa daktari maana natakiwa kurudi ofisini. *sasa ndio naelewa* maana aliniangalia kwa huruma sana huku akivikusanya vikaratasi vile na kuondoka navyo huku akiniambia nisubiri. Alienda kumuita yule daktari aliyeniandikia vipimo.

Jumamosi, 25 Juni 2016

Nimeikatisha ndoto yangu mwenyewe kwa umalaya wangu. Nakumbuka siku ya usaili yule mzungu aliangalia fomu zangu baada ya kunisikiliza na kusoma insha zangu aliniambia, “Young man! If what you have written and have just told us comes from your heart, then I wish you all the best.” 

Nimeikatisha ndoto yangu kwa kuishi maisha mawili. Nakosa hata ujasiri wa kutubu kwa Mungu. Nakosa ujasiri wa kwenda kanisani kesho. Ni nani aliyeniloga?
Pamoja na kupewa ushauri mwingi jana, nimeamua sitokunywa dawa! Nipo tayari kutumikia adhabu niliyojitakia. 

Nilirudi ofisini na kujifanya kama hakuna kilichotokea. Baadaye jioni nilijilazimisha kwenda kuangalia filamu pale LAPF Tower (Movie Night) na kwa maumivu makubwa filamu ile ilikuja wakati wa kuchelewa sana maishani mwangu. Inaitwa ‘God’s Compass’. 

Baada ya kutoka na kuagana na walionialika tena tofauti na siku zote nilikataa kuwapa lift kwenye gari langu na kuwalazimu wajazane wote kwenye gari lingine la mwenzao na kurudi makwao. Nilirudi kwenye gari langu ambapo nilikaa kwa zaidi ya lisaa limoja pale nikilia jinsi maisha yangu yalivyofikia mwisho haraka.

Nimejitahidi kujifanya kama kila kitu kiko sawa kwenye maisha yangu lakini nimeshindwa, nimeishia kulia machozi siku nzima ya leo. Kwa nini Mungu ameruhusu hili linitokee mimi? Kwa nini asingeninyima scholarship na kunipa afya yangu, ningejilipia mwenyewe. Nilikuwa nimeshapanga kuwa kama ningekosa scholarship ningeenda kujilipia pale IFM nisome masomo ya jioni na kwa hakika ningemaliza masomo yangu.

Hii inaweza kuwa hadithi yangu ya mwisho – sikutaraji ingekuwa hii ndiyo hadithi yangu ya mwisho, na iwe ni ya kweli! Lakini niwaombe wote msamaha. Sikuwahi kuamini kama nami ningekuja kuathirika, walikuwa na afya zao, hawakuonekana wameathirika.

Kwa wadada wote mtakaopima na kukutwa mmeathirika kwa sababu yangu – MNISAMEHE. 

Wapendwa, hiki ni kisa changu cha ukweli na ndio maana nimetaja baadhi ya vitu/sehemu za ukweli ili walau muone uhalisia. Kama yote niliyowahi kuyaandika humu yatakosa maana kutokana na nilichokifanya basi naombeni neno langu la mwisho mlizingatie…UKIMWI UPO, NAMI MENTOR NIMEATHIRIKA

Tafadhali msifuate mfano wangu.

Wasalaam na kwaherini,
Mentor.

2 comments:

  1. Huu ni lazima ushuhudia usomaji na kila mtu, nipo hapa kuruhusu ulimwengu wote kujua kuhusu mtu aliyeokoa uhusiano wangu na mtu huyu mkuu anaitwa Dr IZOYA. Hakika alifanya kazi nzuri kwangu kwa kumrudisha mpenzi wangu wa zamani ambaye aliniacha na kuahidi kamwe kurudi kwangu tena. Kwa hili, nimekuja kutambua kuwa kutoa maelezo ya Dk IZOYA kwa ulimwengu utafanya mengi mazuri kwa wale walio na nyumba zilizovunja au uhusiano kwa ajili yake ili kukusaidia kurekebisha uhusiano huo uliovunjika au ndoa yako. Unaweza kumfikia kupitia anwani yake ya barua pepe: drizayaomosolution@gmail.com au kumwita moja kwa moja kwenye [+12098373537]. Kuwasiliana naye na kuona jinsi tatizo lako litatatuliwa ndani ya 24hours. Pia mtaalamu katika mambo yafuatayo ...
    (1) Unataka kurudi nyuma yako.
    (2) Unataka kukuzwa katika ofisi yako.
    (3) Unataka wanaume / wanawake kukufuate.
    (4) Unataka mtoto.
    (5) Wewe ni mjasiriamali na unataka kushinda mikataba
    (6) Unataka mume wako awe wako milele
    (7) Unahitaji msaada wa kiroho.
    (8) Umeshambuliwa na unataka kupona fedha zilizopotea.
    (9) Weka talaka
    (10) Kualika kwa mila ya fedha
    (11) Chagua uchaguzi

    ReplyDelete