Tuesday, May 24, 2016

Mwanayumba: Part II



MWANAYUMBA: PART II

Juni 2015

Ilikuwa siku ya Jumamosi, mwanzoni kabisa mwa mwezi huu wa sita. Nilikuwa nikiendesha gari kutokea baharini kwa kupitia njia hii ya kati ya Ikulu yetu ya Magogoni na Ikulu ndogo ya Zanzibar kama unaelekea hospitali ya Ocean Road. Safari yangu ilikuwa ikielekea Chuo cha Utalii. Nilipofika eneo la round about ile nikitaka kukunja kushoto kuendelea na safari yangu macho – yasiyo na pazia – yalielekea upande wa kulia ambapo kuna lango la kuingilia hospitali hiyo ya Ocean Road.

Niliiona sura ambayo ama kwa hakika haikuwa sura ngeni kabisa machoni pangu. Kutokana na uharaka wa nilichokuwa nikikifuata huko chuoni nilishawishika kutaka kuendelea na safari yangu. Wakati huo huo akili yangu iliniambia niangalie tena kulia kwani ninamfahamu mtu huyo. Hapo ndipo nilipogundua kosa nililokuwa ninalifanya. Kwa muda huo ambao akili yangu ilikuwa ikiwaza yote hayo, gari lilikuwa likijiendesha lenyewe kwani niliposhtuka ilikuwa ni baada ya madereva walio nyuma yangu kupiga honi zisizo na idadi, hawakujua nilitaka kwenda upande upi. Nilijilazimisha kukunja kona ya nguvu na kuzunguka tena round about ile na kisha kwenda kusimama mbele tu ya kibao cha hospitali. 

Nilishuka kwa haraka na kwenda kumfuata binti yule huku akili yangu ikiniambia kwa hakika yule ndiye. Kutokana na tukio lililotokea sekunde chache kabla ya hapo, lilimfanya hata yule binti kusimama na kuhamaki huku akinishangaa kama ambavyo wapita njia wengine walivyokuwa wakishangaa huku wengine wakinitukana na kusema walichoweza kusema. Nilishuka kutoka kwenye gari kwa haraka ili nimuwahi kabla hajaingia hospitalini ndani. 

Mwanay…!” nilijikuta nimekatisha sentensi yangu baada ya kugundua kosa kubwa nililolifanya. Hakuwa yeye! Lakini alifanana sana na Mwanayumba wangu. Duh nilisikitika sana! Na kama kuongezea pilipli kwenye kidonda – au kama wahenga wasemavyo, hakuna msiba usi na wenziwe – nikagundua kosa lingine nililolifanya.

Kumbe vijana wa fursa walipoona nimetoka kwenye gari ghafla walikuja na kuniibia laptop na simu yangu iliyokuwa kwenye gari. Hapo hapo wale wa kufunga tairi wakawa wamefika tayari kufunga tairi za gari langu kwa kuwa nilipaki sehemu mbaya isiyoruhusiwa. Nilibaki nimeduwaa maana niliona wakikimbia na sikujua kama mimi ndo nimeibiwa.

Nilimsalimia yule binti ingawa alionekana sasa na haraka ya kuingia hospitalini. Nilipotaka kurudi kwenye gari ili nichukue kadi yangu nimpatie ndipo nilipogundua hayo niliyoyaandika hapo juu. Ilinibidi nirudi nichukue kalamu na karatasi na kumuandikia, “You remind me of a girl – 0784436***” Nikamuachia na kuondoka kwenda kupambana na wazee wa Halmashauri. Hili tukio mpaka kesho sijawahi kuelewa lilivyotokea; alinisubiri nikaenda kwenye gari pamoja na kwamba hakuwa hata akinifahamu.

Ilikuwa mkasa juu ya mkosi mpaka nikajuta kupitia njia ile kwani sikuwahi kuipitia kabla ya siku hii kwenda chuo cha utalii ambapo nilikuwa nikienda kumpelekea laptop ‘mchumba wangu’ Happy. Laptop ambayo tayari imeshaibwa na alikuwa akiihitaji kwani alikuwa na presentation baadaye siku hiyo.

Nisamehe mamii” Nilianza kujitetea baada ya kufika chuoni hapo na kuonana naye.

Nooo babes, usiniambie umeisahau jamanii” alilalamika Happy. Nilitamani ingekuwa hivyo nikawaza naanzaje kumuelezea laptop ilivyoibiwa?

Unatakiwa kunipa pole kwanza!” Nikaanza kuelezea ambavyo wakati nimetoka ferry nilivyokutana na mgogoro pale usawa wa soko la samaki na wakati nikiangalia upande wa kulia sekeseke lililokuwa likiendelea ndipo niliposhituka kuwa nimeshaibiwa simu na laptop. Alikasirika sana Happy nakumbuka. Nami nilielewa kwani mimi sijawahi kuwa mzembe kiasi kile. 

Jioni nilipokea simu nisiyoitegemea. Ilikuwa kutoka kwenye namba nisiyoifahamu na pamoja na kwamba nilikuwa nime-install application ya ‘true caller’ bado ilishindwa kunijulisha nani alipiga namba ile. Bado nilikuwa na huzuni kwani tukio la mchana bado lilikuwa limeniacha na mchanganyiko wa hisia na Happy aligoma kuja kwangu jioni hiyo.

Niliipokea kwa wasiwasi, “Hello

Hello Mentor.” Ilikuwa sauti ngeni lakini si ngeni, sikutaka tena kujichosha kuwaza ni wapi nimewahi kuisikia, nilisubiri ajitambulishe mwenyewe.

Naam, ilikuwa sauti ya Mwanayumba!!! Mwanayumba…uliipataje namba yangu?

Kumbe, binti yule niliyemfananisha asubuhi alikuwa ndugu yake na kwamba hata yeye mwenyewe alikuwa ndani hospitalini. Alinieleza kuwa baba yake mzazi alikuwa mgonjwa na wapo Dar kwa ajili ya tiba ya baba.
Kumbe, binti yule alipofika ndani hospitali alimsimulia Mwanayumba kisa chote kilichotokea nje hadi kumuonesha karatasi ile nilipoandika namba yangu ya simu. Anasema aliikumbuka wakati uleule alipoiona na kujua kuwa ni namba yangu, akaisave kwenye simu yake na ndo amenipigia.

Alinieleza jinsi gani baada ya sisi kukutana pale Shoprite Arusha aliibiwa simu na tangu siku hiyo amejitahidi kunitafuta bila mafanikio. 

Kiufupi, pamoja na mengine mengi, ameolewa na ana mtoto mmoja, yeye na mumewe wanaishi Arusha. Hapo ndipo paliponirudisha mawazo kwa ndugu yake! Niliumia moyo maana kusema kweli bado nilikuwa na hisia juu yake lakini aliponieleza kuwa ameolewa moyo wangu ulivunjika. Ni kweli sikuwa nimetegemea kuonana naye tena, na nilikuwa nimeshaanza mahusiano mengine lakini kitendo cha kuisikia sauti yake nyembamba yenye kubembeleza kulinikumbusha kipindi kile, 2003, wakati bado tupo kwenye mahusiano.
Nilimuambia asimueleze ndugu yake kama tunafahamiana na akakubali maana tulikubaliana kuwa sasa mimi na yeye hatuna tena ‘future’ pamoja.

Baada ya hapo aliniambia atamshawishi ndugu yake anitafute na kweli kuanzia siku iliyofuata tulianza kuwasiliana kwa ukaribu na huyo ndugu yake bila huyo ndugu kufahamu mchezo aliochezewa.
Nilijikuta katikati ya pembetatu ambayo sikuifurahia. 

Kwenye pembe moja alikuwa Happy ambaye nilianza kuanza kumbembeleza anisamehe kwani lililotokea halikuwa uamuzi wangu, na ni jambo ambalo lingeweza kumtokea mtu mwingine yeyote. Ilimchukua muda kunisamehe maana kazi zake za shule nyingi zilikuwa mule na pamoja na kujitolea kumnunulia nyingine lakini hakufurahia kabisa. Pamoja na hayo, bado alibaki kuwa ‘mchumba wangu’ (naweka kwenye parandesi maana ni mchumba wa mjini, wazazi hawamfahamu, ila ninampenda!) Uhusiano wetu ulipungua nguvu sana katika kipindi hiki jambo lililopelekea kukua kwa pembe nyingine hizi mbili.

Kwenye pembe ya pili, alikuwa ndugu yake Mwanayumba. Huyu tulianza kuwasiliana kimzaha mzaha. Alinielezea walivyonicheka siku niliyomuona na mkasa ulionipata ila alinisifu maana nilionesha ujasiri wa kipekee. Yeye alikuwa akisoma CBE hivyo yeye alikuwepo jijini hapa. Kidogo kidogo maongezi yakaelekea kwingineko. Sitaki kutumia sababu ya ugomvi wangu na Happy kama kigezo lakini ulichangia sana. Tulianza kukutana mara moja moja na siku ambazo Happy alikwenda kumtembelea dada yake huko bara basi alikuja kwangu.

Kwenye pembe ya tatu alikuwa Mwanayumba. Tulikuwa na mambo mengi ya kuzungumza hasa kwa kuwa ilikuwa takribani miaka saba tangu tuonane na mengi yalikwisha tokea hapo kati. Alikuwa ameolewa na wamebahatika kupata mtoto mmoja mpaka sasa. Alinieleza matatizo aliyokuwa nayo kwenye ndoa yake hasa kwa kuwa mumewe hakupenda yeye ajiendeleze kielimu. Yaani ingekuwa ni uamuzi wa mumewe huyo, basi angemwachisha kazi kabisa. Hatukuwahi kabisa kugusia kidonda kilichokuwa kimeshaanza kupona cha mapenzi yetu.

Siku iliyobadilisha mwelekeo wa maongezi yetu ni siku ambayo bila kukusudia wakati tunawasiliana kwa jumbe za simu tulijikuta sote tumetumiana ujumbe unaofanana; “Ila nilikupenda,” ulisomeka ujumbe huo.

Wakati hili linatokea ilikuwa imeshafika mwezi wa nane kama sikosei. Mahusiano yangu na Happy yalikuwa yakielekea kuzuri baada ya muda kutusahaulisha tukio la kuibiwa laptop. Nadhani kilichosaidia zaidi ni kwamba walau alikuwa ameshamaliza chuo na laptop niliyomnunulia; maana ilikuwa mara mbili zaidi bora kuliko yake ya mwanzo…asante JK!

Kilichotokea mwezi huu wa nane, Agosti 2015, ni ubinadamu…naomba msomaji wangu usinihukumu!

Nilichukua likizo ya dharura ya siku 14 tukaenda zetu Morogoro kuwasalimia wazazi wa Happy. Tulikaa kwa siku nne mkoani huko na kurudi zetu Dar wikiendi. Alikuwa akifanya kazi ya kujishikiza katika kampuni moja ya binafsi na kwa kuwa alikuwa bado mgeni alipewa siku saba tu za ruhusa yake hiyo. Hivyo mimi nilibaki na siku nyingine saba za mapumziko peke yangu. Tulipanga mwezi wa kumi na mbili tungeenda wote Moshi na yeye akawafahamu wazazi na baadhi ya ndugu zangu. Tulipanga mengi sana ikiwemo kuanza mipango ya ndoa yetu ifikapo mwakani. Yaliyotugombanisha yalikuwa yameshasahaulika.

Wakati huo huo, nduguye Mwanayumba alikuwa ananisumbua sana kutaka kupafahamu kwangu. Nyumba yangu – enzi za ujana wangu – nilikuwa nikiiita ‘kichinjioni’! Nikabaki najiuliza, ‘sawa nimebadilika na niko kwenye kuelekea hatua kubwa sana maishani mwangu, lakini je, nitaweza kujizuia akija kwangu?
Niliamua liwalo na liwe, sikuwa na mpango wowote na yeye hivyo hata likitokea sitakuwa na deni lolote kwake, nikamkaribisha siku ya Jumanne. Kwa kuwa Happy alikuwa kazini sikuwa na hofu yoyote alipokuja. Sitaelezea yaliyotokea ila yalitokea! 

Jioni wakati namrudisha ferry ili aende kwake nilipokea ujumbe wa simu ulionichanganya. “Mentor, nipo njiani kuja Dar kuchukua dawa za baba. Sijawaambia ndugu zangu kuwa ninakuja leo. Ninahitaji kuongea na wewe leo naomba uje kunipokea Ubungo,” alikuwa Mwanayumba. 

Na kama kuhakikisha kile alichoniambia, nduguye alijikuta akisema tu kuwa Mwanayumba angekuja kesho,  "anakuja kuchukua dawa za baba yake."

Safari ya ferry ikarefushwa kuelekea Ubungo. Huku nyuma nikamwambia Happy kuwa nimevuka naenda kukutana na marafiki zangu na nitachelewa sana kurudi hivyo tusingeonana siku hiyo. Hakuwa na wasiwasi na mimi. Ingawa sikujua lengo la wito huu wa Mwanayumba lakini sikuwa na wasiwasi, nilikwisha jiapia tangu miaka mingi kamwe kutojihusisha kimapenzi na mke wa mtu…hata iweje! Nilijua tu kwa kuwa hakuwa na wakati mzuri na mumewe, alikosa mtu wa kumsikiliza hivyo ni kweli alihitaji tu mtu wa kuongea naye. Sikwenda na maandalizi yeyote!

Nilifika Ubungo na kumpigia simu ambapo aliniambia baada ya kuona ujumbe wangu haujajibiwa aliamua kuchukua chumba na kupumzika. Alinielekeza alipofikia nami bila hiyana niligeuza gari kuelekea kunako hoteli moja pembeni mwa stendi ya mabasi yaendayo mikoani ya Ubungo. Ndiyo, ingawa siikumbuki jina, nakumbuka ipo nyuma ya hostel ya chuo kikuu cha Dar es salaam ya pale Ubungo.

Kwa kuwa sikuwa nimekula na kwamba nilifika mida muafaka kabisa ya kupata chakula cha jioni tuliagiza chakula cha jioni nikimuambia kuwa tutaongea wakati tukila ili tuokoe muda niweze kurudi kwangu, tuue ndege wawili kwa jiwe moja. Naye akapendekeza kama ni hivyo basi tupelekewe chakula chumbani ili tuweze kuongea kwa uhuru. Sikuwa na hofu yeyote nilihisi tu yatakuwa ni maongezi yenye kuhitaji faragha na asingependa watu pale wafahamu mambo yake ya sirini, nikakubali.

Nadhani itoshe kusema kuwa tangu mlango wa kuingia chumbani ulipofungwa nasi kujikuta chumbani wawili tu hadi wakati nilipoufungua mlango kutoka muda wa saa tano ya usiku, sidhani kama tuliongea maneno zaidi ya kumi chumbani humo. Niliondoka kwa aibu kubwa ya kitendo tulichokifanya, nilijijutia, nilijichukia, niliichukia siku hiyo.

Nilirudi kwangu na tangu siku hiyo sikuwasiliana tena na Mwanayumba! Ilikuwa afadhali kuishi hivyo, ilikuwa afadhali kipindi kile nilipokuwa nikimtafuta bila mafanikio. Hata ndugu yake ilinibidi kumueleza ukweli kuwa nina mchumba hivyo tulibaki kuwasiliana kishikaji tu pamoja na kwamba alinikasirikia mwanzoni ila mara moja moja alikuwa akija tunacheza ‘video games’ kwangu…he he he

2016, May 22, Jumapili

Tulikuwa tumetoka ibada ya asubuhi mimi na mchumba wangu Happy. 

Tulirudi nyumbani kwake kwa ajili ya kupata staftahi. Ni wakati huu nikiwa napeleka vihusika sebuleni kutoka jikoni ndipo ulipoingia ujumbe kwenye simu yangu – niliyoiacha jikoni tulipokuwa tukipika na Happy wangu. 

Nilirudi jikoni nikakuta ameshikilia simu huku uso wa simu ukinielekea mimi ili nisome vyema ujumbe uliokuwa umeingia. (Kwa bahati mbaya simu yangu ikiingia ujumbe huwa ujumbe una ‘pop up’ juu ya screen…sijui nielezeeje vyema uelewe)

From: nduguye Mwanayumba
Ujumbe: Mwanayumba amejifungua mtoto anafanana na weweeeeee….

Nilimuangalia Happy usoni kutaka kufahamu yuko kwenye hisia ipi na sikufurahishwa na sura niliyoiona. Ilikuwa ni sura yenye kutaka maelezo. Nitaanzaje kumuelezea! Mwanayumba ni nani? Huyu aliyetuma ujumbe huu ni nani? Kwa nini aniambie kuhusu mtoto wa Mwanayumba? Nianze kumuelezea kutokea wapi? Niruke sehemu ipi? Laptop yake? 

Ngoja kwanza…MTOTO HUYU NI WA NANI? Akili ilihama ghafla hadi kwenye chumba kile, siku ile Ubungo. Hapa ndipo nilipogundua kuwa kichwa cha binadamu ni zaidi ya mashine maana bila kujigusa niliweza kuhesabu miezi na ndipo hapo iliponiingia kichwani. 

HAIWEZEKANI!” nilijikuta nikiropoka kwa nguvu.

Haiwezekani nini Mentor?” aliniuliza Happy. Nilishtuka kutoka kwenye lindi langu la mawazo ya kujitakia na kugundua kumbe nipo na Happy na ninatakiwa kujibu maswali mengi sana ambayo sijui naanzaje kuyaelezea. 

Nilirudi sebuleni huku Happy akija nyuma yangu. Alitaka majibu! Sikuwa na majibu! Ghafla nikaukumbuka wimbo wa zamani wa Shaggy – It wasn’t me! Nilitamani niutumie walau kwa wakati ule niondoke pale nikapate uhakika kwanza wa habari zile. Lakini ningewezaje kusema, “aaah babe atakuwa alikosea tu mtu wa kumtumia ujumbe” wakati nilishapayuka mengine ya zaidi?

Baada ya lisaa lizima la kuelezea maneno yasiyoeleweka nilifukuzwa – na njaa yangu – nikarudi kwangu. Lakini kwanza nikapitia mahali nikapata supu nikampigia simu Mwanayumba lakini hakupokea simu yangu. Nikampigia ndugu yake akanielezea ambavyo mtoto anafanana na mimi yani kama angejua tunafahamiana basi angekuwa na uhakika kuwa mtoto ni wa kwangu. Jambo jema ni hakujua kuwa mimi na Mwanayumba tulikuwa tukifahamiana hata kabla ya yeye. Nilimuomba anitumie picha na akaniahidi atanitumia lakini hadi naandika hapa hatajinitumia na hataki kupokea simu yangu tena.

Mwanayumba, kama utasoma hapa naomba ufahamu umeniumiza tena kwa mara ya pili. Sikutegemea kufanya tulilolifanya lakini pia sikutegemea kupata matokeo tuliyoyapata. Najua umeolewa hivyo sina haki wala dai juu yako lakini ningependa tu kufahamu kama mimi ndiye nilihusika na ujauzito huo au la! 

Mwanayumba umebadili na namba za simu na sijui umemuambia nini mdogo wako hapokei tena simu zangu. Sijui njia nyingine ya kukupata lakini natamani ningefahamu ukweli. Natamani ungeniweka wazi…au tusubiri tena miaka mingine kumi hadi tutakapokutana tena katika mazingira yasiyoelezeka ndipo nitaufahamu ukweli? Nilikupenda kweli ila umeniumiza, ni afadhali nisingekutana tena na wewe…

Wasalaam wapendwa,
Mentor.

No comments:

Post a Comment