NDEGE WA PELIKANA: HADITHI YA
BIBI
Mimi na mama yangu
tuna kitu kimoja tunachofanana. Sote tuna jino moja lililomegeka. Tofauti –
kubwa – huja pale tutakiwapo kuelezea sababu ya kumegeka huko. Nikiwa mdogo
nakumbuka nilikuwa nikimuuliza kwa nini jino lake limemegeka. Alinijibu kuwa
alitaka kufanana na Nyerere vile alivyochonga meno yake. Niliziangalia picha za
Nyerere na kuona kweli ni kama alichonga meno yake ya mbele. Alikuwa
akipendeza.
Nami nilitaka kuwa
kama mama, tatizo sikujua ni jinsi gani alilichonga la kwake na kwa nini yeye
alichonga moja. Kila nilipokuwa nikimuuliza alikataa kunijibu. Alisema nikiwa
mkubwa nitaweza.
Siku moja niliamua
liwalo na liwe na nikaamua na mimi nitamega jino langu kuwa kama la mama.
Nililigonga na jiwe! Maumivu niliyoyapata siku ile siwezi kuyaelezea lakini
ilimchukua hadi bibi kunibembeleza. Aliniuliza kwa nini nilijigonga na jiwe na
baada ya kumwelezea akaniambia ninyamaze anielezee kisa.
Bibi: “Hapo zamani
za kale, palitokea ndege mmoja aliyeitwa ‘pelikana’. Ndege pelikana alipenda kuishi
kando kando ya maji kwani chakula chao kikubwa kilikuwa samaki na mazao ya
majini. Alitotoa mayai yake kipindi cha kiangazi na kuyahifadhi juu kabisa ya
mti kwa usalama wao.
Kwa bahati mbaya,
kiangazi kile kilizidi na kuwa ukame. Mvua hazikunyesha kwa muda mrefu. Hata
makinda yalipototolewa mama pelikana alikuwa akipata shida kusafiri umbali
mrefu majini kutafuta chakula kwa ajili ya wanae. Kwa kuwa walikuwa wengi
hakuweza pia kuwabeba wote ili wahame kutafuta eneo lenye chakula.
Mama pelikana
alijitahidi kukusanya wadudu kidogo waliokuwepo wakati ule kwa ajili ya wanae.
Hata hivyo ukame ulizidi, samaki wote walikufa. Makinda wake walianza kudhoofu
kwa kukosa chakula. Mama pelikana akakosa mbinu mbadala ya kuwalisha wanae.
Alianza kwa kujidonoa
hadi akatoka damu kisha akawapa wanae. Aliendelea kujidonoa kisha kuwalisha
wanae nyama ile itokayo mwilini mwake. Baada ya muda mfupi alikufa. Makinda
yale bila kujua walianza kuudonoa mwili wa mama yao na kuula. Kwa kuwa alikuwa
mkubwa sana makinda yale yaliendelea kuula mzoga wa mama yao hadi ulipokwisha.
Kwa bahati nzuri
mzoga ulipoisha makinda yale yalikuwa yameshakua na kuwa ndege pelikana kamili.
Mvua nazo zilianza kunyesha hivyo kukawa hakuna tena tatizo kupata chakula.
Wale ndege pelikana
walianza kuruka huku na huku wakimtafuta mama yao huku kila wanayekutana naye
wanamwambia mama yao aliwakimbia.
Mimi: Lakini bibi,
si mama yao walimla wenyewe?
Bibi: Hawakujua
kama walimla wao.
Bibi aliniuliza,“Unajua
kwa nini nimekuambia hadithi hiyo?”
Mimi: “Sijui bibi”
Bibi akaendelea
kunisimulia,
“Wakati wewe bado u mdogo sana, ulikuwa mtundu! Ulikuwa ukipenda
kugusa kila kitu. Siku moja katika utundu wako uliingia jikoni na kwa bahati
mbaya ulivuta sufuria iliyokuwa juu ya meza. Kwa kuwa hukuweza kuifikia
ulitumia kitambaa kilichokuwa chini ya sufuria ile. Kwa bahati nzuri mama yako
alikuwa karibu na alipoona kuwa sufuria ile inakaribia kuanguka alikurukia na
kukusogeza mbali na ile sufuria. Ni wakati huo ndipo alipojigonga na mlango wa
kabati na kwa bahati mbaya jino lake likavunjika. Ndani ya sufuria ile kulikuwa
na maziwa ya moto sana ambayo ndiyo kwanza alikuwa ameyaepua kutoka jikoni. “
Ghafla maumivu ya
jino yakanianza upya ikabidi tukatishe hadithi tuanze kubembelezana tena.
Wasalaam wapendwa,
Mentor.
No comments:
Post a Comment